HADITHI

Wednesday, July 22, 2015

HADITHI YA UTAMU WA ZEGE

SEHEMU YA KWANZA



*****
MLIO wa simu yake ndiyo uliozindua kutoka katika ndoto yake ambayo hakuimalizia vizuri. Ndoto iliyoamsha tabasamu zuri kama aamkavyo kila siku akiwa na furaha. Furaha ya kupata kile akitakacho. Maisha aliyatamani na kuweza kuwa nayo.
Hakuwa na jinsi zaidi ya kutii amri ya simu yake. Alijiwekea alamu tayari kwa kumwamsha kila siku. Kaupepo kalichopenya dirishani pia hakikumpa nafasi ya kuendelea kujigubika na shuka. 
Alizitumia kama dakika tano kujiweka sawa kabla ya kutoka kitandani. Usingizi haukumweka tena kitandani. Alitabasamu tena kuushukuru upepo ulioumaliza usingizi wake na kumfanya mpya tayari kwa kuianza  siku hiyo. Alijivuta hadi kushika simu yake iliyokuwa katika kijimeza kidogo pembeni ya kitanda na kuiangalia. Hakukuta chochote zaidi ya nambari zilizoonyesha muda wa kuamka baada ya ile alamu kuisha.
Saa kumi na moja na nusu asubuhi ni muda ambao siku zote alijikuta yuko macho. Wakati mwingine aliiwahi alamu ya simu yake kabla haikulia kumwamsha. Hapo alijua labda ililia na hakuisikia na hivyo amechelewa. Alifurahi mara nyingi alipoiwahi. Alijua kulala sana ni dalili za uvivu na hivyo hakuupa nafasi uvivu umtawale.
Wakati mwingine hakuipenda kwani ingemaliza hamu yake ya kulala wakati bado ana usingizi, hivyo alijua siku za kuiweka na siku za kuitoa. Ni endapo angechelewa kulala sana. Asingeiweka na siku hiyo angeamka muda wowote na kwenda kazini.
Kama kawaida yake. Kioo kilikuwa ni kitu cha pili baada ya kuiwasha taa yake iliyokuwa karibu na kitanda. Taa inayowekwa mezani kwa ajili ya dharura. Mwanga hafifu uliomwangazia ulimtosha kujiangalia usoni peke yake. Alitaka kila siku aone mabadiliko yaliyotokea wakati akiwa amelala. Kama angeona utofauti, hakusita kwenda kwa mtaalamu ili amsaidie. Lakini leo hakuona lolote. Alijiona vilevile kama alivyolala jana yake saa tano na nusu usiku.
Kati ya mambo ambayo Jane aliyahusudu sana ni jinsi alivyo. Alijua ni hulka ya wanawake kujipenda lakini yeye aliona amewazidi kwa kujipenda alivyo. Kitu gani hakuwa nacho hadi asijihusudu mwenyewe pindi ajiangaliapo kwenye kioo chake mwenyewe...
Aliamka sasa na kukifuata kioo kikubwa alichokuwa amekiegemeza ukutani. Inawezekana kwa kuamka mapema kila siku ni ile autumie muda huo kucheza na kioo. Vyumba vyake viwili na maliwato iliyokuwa ndani ilimfanya ajisikie huru kama aishiye katika hekalu. Yote aliyafanya ndani. Alifurahia maisha yake. Alifanya alichokitaka.
Kioo chake hakukitumia vibaya. Sasa ilikuwa zamu ya umbo lake. Alikifuata kioo na kukisimamisha vizuri. Alijiona wote.  Alitoa shuka ambalo alikuwa amejifunika. Alilirusha hadi kitandani kama vile alisahau bahati mbaya akashuka nalo. Alisahau kwamba lilitakiwa limsitiri. Habari hiyo hakuitaka. Alisimama wima. Tabasamu lilianza kuchanua taratibu. Kila ajiangaliapo husahau kama alifanya hivyo jana yake. 
Alijitazama na kuliangaza umbo lake lililoimarika vizuri. Alijitamani. Alishika kiuno chake kwa staili ifanywayo na walimbwende wawapo katika mashindano. Kisha akatembea hatua mbili mbele. Alicheka. Alijikubali. Alitamani apige kelele kumshukuru aliyemleta duniani.
Alirudi tena hatua mbili nyuma. Sasa aligeuka kuangalia umbile lake kwa nyuma. Aliguna akimaanisha Muumba hakumkosea. Taratibu akawa anaelekea bafuni akiwa hajaridhika.
Alilifuata bafu huku macho yake yakiwa nyuma kumalizia kujitazama tena na tena kama hatatoka tena alikokwenda. Huko bafuni yakawa yale yale. Kila kiungo kikisafishwa kwa nafasi yake. Mikono yake laini ilipita kila sehemu kuhakikisha inapata sabuni iliyokuwa inanukia pamoja na maji.
Dakika kumi zilimtosha kujimwagia maji, si mkaaji sana wa bafuni. Alitoka. Alirudi tena kiooni. Sasa ilikuwa ni kujikausha kwa taulo lake jeupe na safi. Alifanya hivyo akilipitisha katika kila kiungo chake. Matiti, shingoni, mapajani na miguuni huku akimalizia mgongoni kwa kulibenua nyuma na kulitembeza sehemu yote ya mgongo. Aliridhika.
Alilifuata kabati lake na kutoa nguo. Kioo hakikuwa mbali. Alikifuata na kucheza nacho tena kama pacha wake. Alicheka mwenyewe.
Alijiona amependeza. Alitembea kwenda mbele na kurudi nyuma. Mwishowe alijiona mjinga. Alikimbilia simu yake na kuzima taa tayari kufunga mlango na kuelekea kazini kwake.
 USIKOSE SEHEMU YA PILI

No comments:

Post a Comment